Thursday, December 22, 2011

Wasiwasi bado mkubwa Dar es Salaam


Wasiwasi bado mkubwa Dar es Salaam

 22 Disemba, 2011 - Saa 14:46 GMT
Dar es Salaam
Hali ya wasi wasi bado inazingira maeneo ya mabondeni katika jiji la Dar Es Salaam kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha kusababisha vifo vya watu wasiopungua 20 na uharibifu mkubwa wa mali na miundombinu.
Idara ya utabiri wa hali ya hewa (Tanzania Meteorological Agency) imeonya kuwa mvua hizo nzito zitaendelea kunyesha na imeshauri watu wanaoishi maeneo ya mabondeni kuhama haraka.
Mvua hizo zilizoanza kunyesha Jumanne alfajiri zimesababisha shughuli nyingi kusimama hasa kutokana na barabara muhimu zinazounganisha jiji na vitongoji vyake kutopitika na madaraja kubomoka.
Baadhi ya maeneo yaliyoathirika zaidi ni kama Jangwani, Kigogo, Mburahati na Bonde la Mto Msimbazi ambalo linamwaga maji katika bahari ya Hindi.
Kutokana na kiasi kikubwa cha maji kuingia baharini, hata maji katika Bahari ya Hindi yamebadilika rangi na kuwa ya maji machafu ya mafuriko.
Kuna maelfu ya watu wanaoishi katika maeneo ya mabondeni ambao mpaka sasa makazi yao yamebomolewa na wamekuwa wakihifadhiwa katika vituo vya dharura.

Kamanda wa polisi mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova

"Tulikwenda kuwaokoa baadhi yao na waligoma kuhama wakisema hawawezi kuondoka kwa kuwa wanachunga mali zao"
Shirika la msalaba mwekundu linakadiria kuwa watu zaidi ya 5,000 wameathirika kwa njia moja au nyingine kwa kukosa makazi au miundombinu kuharibiwa.
Mmoja wa waathirika ni Tabu Kibwa aliyeieleza BBC kuwa nyumba yake yote imezingirwa na kumezwa na maji.
"Tumepoteza kila kitu, kwa kweli tumebaki mikono mitupu. Kila kitu katika nyumba kimepotea ikiwa ni pamoja na televisheni na majokofu," aliileza BBC.
Hata hivyo wengi wa wakazi hao wamegoma kuhama kwa miaka mingi licha ya kufahamishwa hatari ya mafuriko.
Kwa mujibu wa Idara ya hali ya hewa, hizi ni mvua nzito zaidi kuwahi kunyesha Dar Es Salaam tangu Tanzania ilipopata uhuru mwaka 1961.
Kamanda wa polisi wa mkoa maalum wa Dar es Salaam, Suleiman Kova, amewasihi watu kuhama mabondeni, lakini amekiri baadhi yao wamegoma kabisa.
"Tulikwenda kuwaokoa baadhi yao na waligoma kuhama wakisema hawawezi kuondoka kwa kuwa wanachunga mali zao,” alisema.
Ingawa mvua zimeonekana kusababisha maafa makubwa zaidi Dar Es Salaam, lakini zimekuwa zikinyesha kwa nguvu katika maeneo mengi kama Iringa na Rukwa ambako madaraja na barabara vimebomolewa.

No comments:

Post a Comment