Monday, December 19, 2011

Jeshi la Marekani laondoka Iraq

Jeshi la Marekani laondoka Iraq

 18 Disemba, 2011 - Saa 10:05 GMT
Wanajeshi wa mwisho wa Marekani nchini Iraq sasa wameshaondoka kabla ya siku ya mwisho wa mwaka, ambao ndio wakati uliokubaliwa baina ya Iraq na Marekani.
Jeshi la Marekani likiondoka Iraq
Gari la jeshi la mwisho lilivuka mpaka na kuingia Kuwait asubuhi mapema, na kumaliza vita vya Iraq vya karibu miaka 9, muda mrefu kushinda ilivotarajiwa awali.
Msafara wa mwisho wa matingatinga kama 110 uliwasili Kuwait, ukishangiliwa, na wanajeshi kukumbatiana.
Msafara huo ulikuwa na wanajeshi 500 wa mwisho wa Marekani kuondoka Iraq.
Katika vita vya Iraq Marekani ilipoteza karibu wanajeshi 4500 na zaidi ya 30,000 walijeruhiwa.
Inakisiwa raia zaidi ya laki moja wa Iraq waliuwawa, na haijulikani wangapi wameachwa na vilema katika mitibuko ya nchi hiyo.
Sasa Wamarekani wanaondoka, lakini Marekani itaendelea kuwa na madaraka kupitia ubalozi mkubwa ambao utakuwa piya na maafisa wa kijeshi 150 wataoshughulikia biashara ya silaha kwa Iraq; pamoja na raia mia kadha wa kuwafunza wanajeshi wa Iraq namna ya kutumia vifaa vya Marekani.


Bunge la Iraq lagawanyika

 17 Disemba, 2011 - Saa 18:20 GMT
Pande kubwa kabisa la wabunge wa Iraq limetoka kwenye ukumbi wa bunge, ili kulalamika juu ya mamlaka mengi aliyonayo Waziri Mkuu, Nouri al-Maliki katika uamuzi wa serikali.
Waziri Mkuu wa Iraq, Nouri al_maliki
Kundi hilo liitwalo Iraqiya, ambalo halielemei kwenye dini, na la waziri mkuu wa zamani, Iyad Allawi, limeitia nchi katika msukosuko wa kisiasa, siku chache baada ya wanajeshi wa Marekani kuondoka.
Kundi hilo lenye robo ya viti 325 vya bunge, limetaka kufanywe mazungumzo na serikali inayoongozwa na Washia, ili kutatua swala hilo.
Iraqiya ilishinda karibu kura zote za Wasunni wa Iraq, ambao ni wachache.

Iraq yajaribu kupatanisha Syria

 17 Disemba, 2011 - Saa 15:34 GMT
Ujumbe wa serikali ya Iraq umekwenda Syria, kuisihi serikali iache kutumia nguvu nchini humo.
Maafisa wa Iraq na Syria
Ujumbe huo unaongozwa na Waziri wa Usalama wa Iraq, Falah al-Fayadh, na unasema kuwa unawasiliana na upinzani wa Syria pamoja na serikali.
Wairaqi wanajaribu kupatanisha ili kufanywe mazungumzo yatayofuata mapendekezo ya amani yaliyotolewa na Jumuia ya nchi za Kiarabu.
Mwandishi wa BBC anasema, Wairaqi wanafikiri wanaungwa mkono na Marekani katika juhudi hizo, na haikuelekea kuwa watafanya ziara hiyo bila angalau kuungwa mkono na Iran.
Ziara hiyo inafanywa wakati kundi kuu la upinzani la Syria - Syrian National Council -- linakutana Tunisia.
Linatarajiwa kujadili mkakati wake wa kujitayarisha kama serikali kivuli, tayari kuchukua madaraka Rais Assad akiondoka.

No comments:

Post a Comment